Mbunge wa Changamwe Omar Mwinyi [Osman Suleiman]

Do you have a lead on a newsworthy story? Share news tips with us here at Hivisasa!

Mbunge wa Changamwe Omar Mwinyi ametoa ushahidi wake kwa mara ya kwanza kwenye kesi ya kupinga ushindi wake wa uchaguzi wa Agosti nane wa mwaka jana.

Kesi ya kupinga ushindi wake iliwasilishwa mahakamani na mgombea kiti cha ubunge kutipitia chama cha Jubilee Abdi Daib.

Akitoa ushahidi wake siku ya Jumatano,Mwinyi alipinga kuweko kwa wizi wa kura katika eneo bunge hilo na kuongeza kuwa uchaguzi ulikuwa wa uwazi na wa haki.

Mbunge huyo aliambia mahakama kuwa hakuhusika kamwe katika kushurutisha maafisa wa tume ya uchaguzi ili waweze kumtangaza mshindi kama inavyo daiwa na mpinzani wake Daib.

Mwinyi ameyataja matokeo yaliyowekwa kwenye tovuti ya tume ya uchaguzi kama yasiyikuwa ya ukweli na kusisitiza kuwa matokeo halali ni yale yaliandikwa kwenye fomu 35b ambayo ndio ilitumika kutangaza mshindi wa kiti hicho.

Kwenye fomu 35B Mwinyi alipata kura alipata kura 31,584 ilhali kwenye tovuti ya IEBC ilionyesha kuwa alipata kura 31,322.

Mwinyi aliambia mahakama kutupilia mbali kesi hiyo kwa kuitaja kama isiyokuwa na msingi wowote wa maana,ikizingatiwa wakazi wa Changamwe walimchagua kwa moyo mmoja.

Kulingana na ushahidi wa Abdi Daib ni kwamba Omar Mwinyi aliongezewa kura 262 katika uchaguzi huo wa Agosti 8 ambapo kulingana na fomu 35B iliyowasilishwa mahakamani, Mwinyi alipata kura 31,584 kinyume na kura 31,322 ambazo zilitumwa kwenye mtandao wa matokeo ya tume ya IEBC.

Daib aliitaja hatua hiyo kama njama ya wizi.

“Huu ni wizi wa wazi uliofanyika katika vituo vingi eneo la Changamwe ili kumpitisha Omari Mwinyi,” alisema Daib.

Ushahidi wake ulionyesha kuwa kura zilizoharibika kulingana na Fomu 35B ni kura 494, kinyume na zile zilizotumwa kwenye mtandao wa IEBC ambao ulionyesha kura 1,120.

Daib alitilia shaka tofauti hiyo na kuitaja kama njama ya wasimamizi wa kura hizo kutekeleza wizi.

“Tofauti hii ni ishara kuwa uchaguzi huo haukuwa wa uwazi na huru,” alisema Daib.

Aidha, picha na nakala ya kifaa cha KIEMS zilizowasilishwa mahakamani zilionesha tarehe ya uchaguzi kuwa Januari 2, 2009 wala sio Agosti 8, 2017.