Mbunge wa Kisauni Rashid Bedzimba amewashtumu maafisa wa Kenya Ports Authority (KPA) na Kenya Revenue Authority (KRA) kwa kuifunga kampuni ya Auto Port, na kusababisha zaidi ya wakaazi 500 kukosa ajira.
Akiongea na wanahabari baada ya kutembelea wafanyikazi wa kampuni hiyo katika eneo la Shamanzi mjini Mombasa siku ya Ijumaa, Bedzimba alisema kuwa hatua waliyochukua maafisa wa KPA na KRA ni ukiukaji mkubwa wa sheria za nchi, pamoja na sheria za Leba na lazima hatua za kisheria kuzingatiwa.
Bedzimba alisema kuwa kufungwa kwa kampuni hiyo kumechangia kusitishwa kwa hudumu nyingi za upakuaji na ukaguzi, pamoja na ukamilishaji wa usajili wa magari ya wateja wa kampuni hiyo.
Aliwataka wasimamizi wakuu wa halmashauri hizo kuliangazia swala hilo ili shughuli za kawaida kurejea.
“Tunawataka wasimamizi wakuu wa Halmashauri hizo za KPA na KRA kuingia kati na kusuluhisha tatizo hilo, Idadi kubwa ya vijana kwa sasa wamesimamishwa kazi na hali kama hiyo huchangia uhalifu miongoni mwa jamii,” alisema Bedzimba.
Mbunge huyo wa Kisauni alisema kuwa ataungana na familia ya Gavana wa kaunti ya Mombasa Hassan Joho wanaomiliki kampuni hiyo ya Auto Port, na kuelekea mahakamani kupinga hatua ya maafisa wa KPA na KRA kufunga shughuli za kapuni hiyo.