Huku kongamano la uwekezaji na biashara likifika ukingoni siku ya Jumamosi, sekali ya kaunti ya Kisii imepewa changamoto ya kutumia nafasi hiyo na kushawishi wawekezaji waliohudhuria kongamano hilo ambalo lilianza siku ya Alhamisi wiki jana.
Akiongea kwenye kongamano hilo siku ya Jumamosi katika uga wa michezo wa chuo kikuu cha Kisii, mfanyabiashara maarufu nchini Chris Kirubi alimwambia gavana wa kaunti hiyo James Ongwae kuweka mikakati madhubuti na kuwapa nafasi vijana walio na ubunifu kutoka kaunti hiyo nafasi ya kupanua mawanda ya taaluma zao.
Kirubi aidha alimshauri gavana Ongwae kuwekeza katika vyuo anuwahi na taasisi za kiufundi kwenye maeneo na miji mbali mbali ya kaunti hiyo ambayo imechipuka kwa kasi kwa masuala ya uchumi wa eneo zima la Nyanza.
Kwa upande wake, gavana Ongwae aliwahakikishia washiriki pamoja na wakazi ambao walifuatilia kongamano hilo kwa siku tatu kwenye vyombo vya habari kuwa atafanya juhudi ili kuafikia azimio la kuifanya kaunti hiyo kuimarika zaidi kiuchumi.
Kwenye kongamano hilo, vijana watatu walijinyakulia zawadi ya kati ya shilingi elfu 250, elfu 500 na milioni kwa kuwasilisha vitengo bora zaidi kwenye ubunifu wa wazo la kibiashara ambapo mama Askah Kerubo aliibuka mshindi wa shilingi milioni moja kwa kubuni nafasi za kazi kupitia utengenezaji wa vibanzi maarufu kama 'Matoke Crisps'.