Share news tips with us here at Hivisasa

Waziri wa fedha katika kaunti ya Nyamira John Omanwa amesema serikali ya kaunti hiyo imetenga millioni 30 ili kununua gari za kuzima moto kama njia mojawapo ya kukabili visa vya mikasa ya moto.

Hii ni baada ya bweni la wanafunzi 40 katika shule ya wavulana ya Nyamira kushika moto siku ya Jumanne mwendo wa saa nane mchana, na kusababisha hasara kubwa ya thamana isiyojulikana.

Moto huo ulianza wakati wanafunzi walikuwa darasani, huku wanabodaboda na wakaazi wakijaribu kuzima moto huo lakini juhudi zao zikagonga mwamba na hawakuokoa chochote katika mkasa huo.

Akizungumza na waandishi wa habari siku ya Jumanne afisini mwake katika mji wa Nyamira baada ya mkasa huo, Omanwa alisema serikali ya kaunti hiyo sasa imetenga pesa ambazo zitatumika kununua magari ya kuzima moto ambayo yamekuwa yakikosa kwa mda mrefu sasa.

“Mikasa imekuwa ikishuhudiwa katika kaunti hii maana hatukuwa na magari ya kuzima moto, lakini sasa wananchi wa kaunti hii watafurahia maana tutanunua magari hayo kwa mda usiokuwa mrefu kwanzia leo,” alisema Omanwa.

Serikali ya kaunti ya Nyamira imekuwa ikikoselewa kwa mda mrefu kwa kukosa magari hayo, jambo ambalo limepelekea uongonzi wa gavana wa kaunti hiyo John Nyagarama kukosolewa kila wakati.