Do you have a lead on a newsworthy story? Share news tips with us here at Hivisasa!

Baadhi ya wakazi wa Kaunti ya Kisii wamejitikeza kukikosoa kitendo cha Wawakilishi katika bunge la Kisii cha kufunga ofisi ya Karani na ile ya msimamizi wa idara ya fedha.

Haya yanajiri baada ya Wawakilishi wa kaunti hiyo kufunga ofisi hizo mbili kwa kile walichokisema ni kucheleweshwa kulipwa marupurupu yao.

Wakizungumza leo na Waandishi wa habari katika mji wa Kisii, wakazi hao wamewakosoa vikali Wawakilishi hao huku wengi wao wakikiri kuwa ni kukosa heshima kwa kufunga ofisi za serikali na kusema wangefuata njia iliyo bora kupokezwa pesa zao bali siyo kufunga ofisi hizo kwani huenda miradi ya maendeleo kutatizwa kwa muda.

“Sasa vile walifunga ofisi hizo walipata hizo pesa? Sisi tunahitaji Wawakilishi walio na maarifa na kufuata pesa zao kwa njia iliyo bora,” alihoji Cleophas Mose, mkazi.

Ofisi ambazo zilifungwa jana ni ya karani wa bunge la kaunti hiyo James Nyaboga na ile ya msimamizi wa pesa Joseph Amenya huku Wawakilishi hao wakidai kuwa hawajalipwa marupurupu ya vikao vya mwezi wa sita.

Kwa upande wake, karani Nyaboga alisema hawana kosa lolote hayo ni madai tu ya Wawakilishi hao kwani walipokezwa mshahara yao ya marupurupu ilivyotakiwa baada ya kuhudhuria vikao.

Hapo mbeleni Wawakilishi walisusia baadhi ya vikao vya mwezi wa sita kwa kutolipwa marupurupu yao.