Wagonjwa katika Hospitali ya Rufaa na Mafunzo ya Kisii wameiomba serikali ya kaunti kupunguza gharama ya dawa katika hospitali hiyo.
Wito huo umetolewa baada ya wagonjwa hao kudai kuwa duka la kuuza dawa katika hospitali hiyo linauza dawa kwa bei ghali.
Wakizungumza na mwandishi huyu siku ya Jumapili katika hospitali hiyo, Gladys Orure, aliyekuwa na mgonjwa alisema baada ya kuhudumiwa, alitumwa kununua dawa lakini bei ya dawa aliyoambiwa anunue ilikuwa ghali sana.
“Mimi nilikuja kutolewa jino kisha nikaagizwa kununua dawa na nilipoenda kununua dawa hiyo, nikaambiwa nilipe 450. Si mara yangu ya kwanza kutolewa jino. Katika zahanati za kibinafsi dawa hiyo huuzwa 150. Kwanini bei iwe ghali katika hospitali ya serikali? Tunaomba serikali iingilie kati ili tusiwe tunasumbuliwa na bei ghali ya dawa,” alisema Chris Bosire, mgonjwa.
Wakazi hao wameiomba serikali ya kaunti ya Kisii kuingilia kati na kulisuluhisha jambo hilo ili wakazi waweze kufurahia huduma bora za afya.