Serikali ya kaunti ya Kisii imeombwa kuwahusisha wakazi wa kaunti hiyo kwa miradi ya maendeleo inayofanywa ili kuonyesha uwazi wa utumizi wa pesa za serikali.
Wito huo umetolewa baada ya kubainika kuwa mara nyingi serikali ya kaunti hudai kufanya maenedeleo bila kuwahusisha wakazi ambao ni watozwa ushuru wanaostahili kusema lile wanahitaji kufanyiwa
Akizungumza na mwandishi huyu siku ya Jumapili mjini Kisii, mwenyekiti wa wafanyibiashara mjini humo Walter Kiyondi alisema serikali ya kaunti inastahili kuwajumuisha wakazi wakati inapofanya miradi ya maendeleo ili kuonyesha uwazi wa utumizi wa pesa zao.
“Naomba kila wakati serikali ya Kaunti ya Kisii inapofanya mradi wowote wa maendeleo iwe inajumisha wakazi ili ukweli kubainika,” alisema Kiyondi.
Kiyondi aliongeza kuwa kuna baadhi ya miradi ya maendeleo serikali hiyo ilisema imefanya ambayo wakazi hawakujumuishwa kamwe.
Wakati huo huo, Kiyondi aliomba wawakilishi wadi wote wa kaunti hiyo ya Kisii kufanya kazi waliochaguliwa kufanya ya kuhakikisha miradi ya maendeleo imekamilika katika wadi zao kabla ya serikali kutoa ripoti kuwa imefanya ili maendeleo kuafikiwa kwa wakazi wa kaunti hiyo.
“Naomba wawakilishi wadi kujaribu kila wawezalo kuhakikisha wakazi wamenufaishwa kimaendeleo katika wadi zao maana bila wawakilishi wakazi hawawezi faidika kimaendeleo,” aliongeza Kiyondi.