Is there a story unfolding in your community? Let Hivisasa know

Baadhi ya wakazi na wakereketwa wa kisiasa katika Kaunti ya Mombasa wameunga mkono Seneta Hassan Omar na kusema kuwa kila mwanasiasa ana uhuru wa kujieleza na hata kugombea kiti kikatiba.

Haya yanajiri huku wanasiasa na wabunge katika kaunti hiyo wakiendelea kumshutumu seneta huyo kufuatia matamshi yake ya hivi majuzi kuwa bunge hilo linatumika na Gavana Hassan Joho kupitisha miswada inayomnufaisha yeye binafsi.

Jabez Oduor, mwakilishi wa Wadi ya Kongowea amemuunga mkono seneta huyo huku akitaja madai hayo kuwa ya kweli.

Akiongea siku ya Jumanne katika kikao na wanahabari, Oduor aliwataka wawakilishi wadi hao kutoshinikizwa na yeyote na kupitisha miswada inayowafaa wananchi kwa jumla.

Musikari Daniel, mkazi wa Likoni, alisema kuwa inaonekana kuwa bunge hilo linatumika vibaya.

"Kuna huu mswada uliopitishwa wa kumpa gavana nguvu ya kuyapa majina barabara za mjini na majumba vilevile. Kwa upande wangu, mswada huo hauna manufaa yoyote kwa wakazi," alisema Musikari.

Otieno Jared, mkazi, aliunga mkono matamshi ya Musikari na kusema kuwa wawakilishi hao wanafaa kufahamu kuwa wapo bungeni kumtetea mwananchi wa kawaida na sio vinginevyo.

Uhasama baina ya Seneta Omar na Gavana wa Mombasa Hassan Joho umeendela kushuhudiwa baada ya seneta huyo kutoa madai ya ufisadi na utepetevu katika serikali ya Kaunti ya Mombasa.

Seneta huyo ametangaza azma yake na kujitosa katika kinyanganyiro cha ugavana ifikapo mwakani katika uchaguzi mkuu.