Wakaazi wa wilaya ya Masaba Kaskazini eneo bunge la Kitutu Masaba wameipongeza serikali ya kitaifa kwa kukarabati barabara ya kutoka Metamaywa hadi Kebiringo.
Wakiongea leo katika kituo cha magari cha Keroka baadhi ya wanabiashara na madereva wamesema punde tu ujenzi huo utakapokamilika watafaidika kwa kuwa barabara hiyo itarahisisha shughuli za uchukuzi.
Peter Ondieki mmoja wa madereva katika eneo hilo amesema wamekuwa wakisumbuka kwa miaka mingi hasa nyakati za mvua.
Lakini kwa sasa Ondieki anasema kuwa watapata afueni kwani shida hiyo itazikwa katika kaburi la sahau.
“Wakati wa msimu wa mvua mimi kama dereva husimamisha shughuli zangu kwani barabara hii haipitiki,” asema Ondieki.
Erick Mokaya, mwanabiashara, asema kuwa watakuwa wafaidi wakuu punde tu itakapokamilika.
“Barabara hii inaunganisha soko tatu kwa hivyo itakuwa ya umuhimu itakapokamilika,” asema Mokaya.
Kwa sasa Mokaya anasema kuwa ukarabati huo utainua kiwango cha maendeleo katika upande huo.
"Biashara zitaweza kuinuka wakati barabara itakopomalizika. Wakulima wengi hupata hasara bidhaa zao zinapoharibikia shambani hasa nyakati za mvua lakini kwa sasa wanabiashara watazichukua kwa urahisi,” aongeza Mokaya.
Aidha maderava wa kituo cha Keroka wameipongeza Serikali ya kaunti ya Nyamira kwa kukarabati kituo cha Keroka jambo ambalo limewarahisishia kazi ya uchukuzi.