Wanafunzi wote waliomaliza mitihani ya kidato cha nne na darasa la nane wameshauriwa kutojihusisha na masuala ya uhalifu, usherati na unywaji wa pombe ila kusubiri matokeo ya mitihani na kuendelea na masomo.
Wito huo umetolewa baada ya kubainika kuwa wengi wa watoto wanapotoka na huaribika kwa kujihusisha na unywaji wa pombe, usherati na uharibifu.
Akizungumza mjini Nyamira siku ya Ijumaa, msimamizi wa watoto katika kaunti ya Nyamira Samuel Masese aliwashauri watoto hao kutojihusisha na maswala ya usherati, kunywa pombe na uhalifu ila kusubiri matokeo ya mitihani na kuendelea na masomo ambayo yatawasaidia siku zijazo.
“Naomba kila mwanafunzi aliyemaliza mtihani asiharibu maisha yake kwa kufanya vitu ambavyo si vya kufurahisha, kila mmoja asubiri matokeo ya mtihani ili aendelee mbele,” alisema Masese.
“Badala ya kufanya vitu vya aina hiyo, wale ambao wanahitaji kujua tarakilishi naomba mwende msomee tarakilishi mnaposubiri matokeo ya mitihani,” aliongezea.
Pia msimamizi huyo aliwahimiza wazazi wote kuwa katika mstari wa mbele kuwapa mafunzo watoto wao ili wasijihusishe na maswala ambayo yataaribu maisha yao.
“Naomba wazazi wenzangu kuwapa mafunzo watoto ili wasije wakajihusishe na maswala ya kunywa pombe na kujiingiza katika usherati ambao utaaribu maisha yao,” aliongeza Masese.