Serikali ya Kaunti ya Mombasa kupitia Wizara ya Barabara na Miundo Misingi imeahidi kurekebisha mabomba ya maji taka katika kaunti hiyo, ili kuzuia kuchipuka kwa mkurupuko wa maradhi.
Akizungumza mjini Mombasa siku ya Ijumaa, wakati wa kukagua shughuli ya urekebishaji wa mabomba ya maji taka inayotekelezwa na maafisa wa kitengo cha majanga katika Kaunti ya Mombasa, Mkuu wa Idara ya Barabara Taufiq Balala, alisema kuwa ili kuwakinga wakaazi dhidi ya kuambukizwa magonjwa ya kiafya yanayosababisha na mazingira duni, lazima shughuli hiyo kutekelezwa kwa dharura.
Balala alisema kuwa maafisa hao watarekebisha mabomba yote ya maji taka ili kuhakikisha wakaazi wa Kaunti ya Mombasa wanaishi katika mazingira safi.
Alisema kuwa hali inayoshuhudiwa kwa sasa katika kaunti hiyo ni duni mno na kadri mvua inavyozidi kunyesha, ndivyo afya ya wakaazi itavyozidi kuwa katika hatari zaidi.
"Tunawaahidi wakaazi wa Kaunti ya Mombasa kuwa mazingira ya Mombasa yatahifadhiwa na kuwa safi zaidi, ili kuhakikisha kuwa hakuna maradhi yoyote ya kiafya yanachipuka kufuatia hali duni ya kimazingira inayosababishwa na mvua inayonyesha,” alisema Balala.
Hatua hii inajiri kufuatia wakaazi wa Kaunti ya Mombasa kushtumu serikali ya kaunti kwa kushindwa kukarabati mabomba ya maji taka.