Msanii nyota wa Pwani Yusuf Kombo al maarufu Susumila, amesema kuwa anafanya fani ya muziki kama kazi wala sio ili kujihusisha katika masuala ya anasa.

Do you have a lead on a newsworthy story? Share news tips with us here at Hivisasa!

Susumila amesema kuwa wengi wa wasanii hutitosa katika muziki wakiwa na malengo tofauti, ila wengi wao huwa wanaingia kwenye fani hiyo ili kutafuta umaarufu na kupata vidosho.

Akizungumza na mwandishi huyu mjini Mombasa siku ya Ijumaa, msanii huyo alisema kuwa alianza fani hiyo kwa malengo ya kujiendeleza kimaisha na kwa sasa anafurahia matunda yake.

Alisema kuwa ukifanya kazi yako kwa bidii, umaarufu utakuja wenyewe na msanii hatalazimika kuutafuta.

“Nani asiye mjua Susumila Mombasa, Kenya na hata Afrika Mashariki kwa ujumla? Umaarufu wangu unakubalika kote kwa ajili ya kazi nzuri ninayoifanya,” alisema Sususmila.

Msanii huyo aliweza kuwika kwa vibao vingi akiwa anakosoa serikali na sasa ameingilia muziki wa kutumbuiza mashabiki wake kwa ngoma za kunengua viungo.

Susumila amewashauri vijana kuwa na mwelekeo wa kimaisha na kutia bidii katika kile wanachokifanya na kuasi maisha ya anasa.