Licha ya pingamizi nyingi zilizoambatana na zoezi la kuwatorosha wachuuzi kutoka katikati ya mji wa Nakuru, matokeo mazuri yameanza kudhihirika.
Zoezi hili ambalo limewaacha wengi bila mahali pa kufanyia biashara zao limewafurahisha wafanya biashara wengi ambao wamekomboa maduka ndani ya mji.
“Kwa muda mrefu, wachuuzi mamenisumbua sana kwani wamekua wakitandika bidhaa zao hata kwenye kiingilio cha duka langu. Mwingine anauza bidhaa zilezile ambazo mimi ninaziuza na kwa vile halipi kodi ya nyumba na ushuru kwake uko chini, hata siwezi kushindana naye,” anasema mfanya biashara mmoja anayefanya biashara ya kuuza vyombo vya stima katika barabara ya Kenyatta Avenue na ambaye hakutaka jina lake litajwe.
Kando na hayo, misongamano katikati ya mji imepungua sana. Watu wanaweza kutembea bila kusongamana kama ilivyokuwa kawaida hapo mbeleni na hata nafasi za kuegeshea magari zimeongezeka.
Tangu kufunguliwa kwa soko la Wakulima Market na Gavana wa kaunti ya Nakuru hapo juzi, wachuuzi wote waliokuwa wakifanyia biashara zao kwenya barabara iliyo nje ya soko kuu la wakulima wameingia ndani na barabara imebaki wazi kwa magari na wanaotumia njia hiyo kwa miguu.
“Yenyewe hapa jam ilikuwaga noma. Hata kupita na mzigo ilikuwa shinda sababu ya msongamano. Angalau sasa tumepata afueni,” kijana anayejiita Mose na anayefanya kazi ya kubeba mizigo kutoka sokoni hadi steji ya magari alimwambia mwandishi.
Eneo lingine lililopata afueni baada ya kufurushwa kwa wachuuzi ni bustani ya Lions’ Garden. Kwa muda mrefu, eneo hili ambalo limetengewa wananchi wajifinjari lilikuwa limevamiwa na wachuuzi wa bidhaa mbalimbali. Ua lote la bustani hili ambalo liko mkambara na barabara lilikuwa mahali pa kuuzia nguo na hata hungeona ndani. Mkaaji mmoja wa Nakuru alionekana kushangaa alipoiona bustani hili.
“Ala! mimi hudhania hapa iko soko. Kumbe ni uwanja wa kupungia hewa!” alisikika akisema Mkaaji huyu.