Polisi kaunti ya Nakuru wanamsaka dereva wa basi ambalo lilihusika kwenye ajali iliyosababisha vifo vya watu wanne.
Dereva huyo alikuwa akiendesha basi hilo kuelekea jijini Nairobi wakati ambapo aligongana na matatu hiyo ana kwa ana.
Wanne hao walifariki papo hapo huku abiria wengine wakikimbizwa hospitalini.
OCPD wa Gilgil Serah Koki alisema dereva wa basi hilo alitoweka pindi tu baada ya mkasa huo.
“Tunamtafuta dereva huyo kwani alitoweka baada ya ajali,” alisema Koki.
Aidha Koki aliitaka kampuni ambayo basi hilo linatoka kusaidia polisi katika uchunguzi wa kisa hicho.
Madereva wametakiwa wawe waangalifu ili kuzuia ajali zinazoweza kuepukika.