Shule ya Upili ya Nyamachani iliyoko wilayani Nyamira Kaskazini, kaunti ya Nyamira, ilifadhiliwa na vitabu vya kusoma na mhisani Charles Mochama.

Is there a story unfolding in your community? Let Hivisasa know

Akizungumza mnamo siku ya Jumapili katika uwanja wa shule hiyo, mhisani huyo Charles Mochama, alifadhili shule hiyo na vitabu vya kusoma ambavyo viligharimu shillingi 50,000 ili wanafunzi wapate fursa ya kusoma kwa bidii na kupita katika mitihani ya kitaifa. 

Wakati huo huo, mhisani huyo aliomba serikali ya kaunti ya Nyamira kushirikiana na serikali kuu kutafuta mbinu mbadala ya kuwatia walimu motisha wakati wanafunzi wanapopita mtihani .

“Walimu ambao somo lao linafanywa vyema katika shule wanastahili kuzawadiwa ili kila mwalimu ajitahidi wakati anawafunza wanafunzi. Kila mwalimu akiwa na motisha, wanafunzi wote wa kaunti hii watakuwa wanapita na viwango vya masomo vitainuka zaidi katika kaunti yetu,” alisema Mochama.

Aidha, mhisani huyo aliwaomba walimu wote wakuu wa shule za kaunti hiyo kujiunga pamoja na kuzungumzia jinsi watakavyo fanya ili wanafunzi wa kaunti hiyo wawe wanapita katika mtihani.

Naibu wa mwalimu mkuu wa shule hiyo Sam Omosa, aliwaomba wazazi wote kushirikiana na walimu ili kuinua viwango vya masomo haswa kwa watoto wao.

“Sisi walimu hatuwezi saidia wanafunzi katika masomo tukiwa peke yetu. Nawaomba wazazi mshirikiane na walimu tuhakikishe wanafunzi hawa wanafanya vizuri katika masomo,” alisema Omosa.