Wanabiashara wanaouza madawa ya kulevya karibu na chuo kikuu cha Kisii wameombwa kuachana na biashara hiyo au kuchukuliwa hatua za kisheria.
Akiongea Ijumaa katika chuo kikuu cha Kisii afisa mwandalizi wa mafunzo katika tume ya kupambana na madawa ya kulevya NACADA Adrian Achenga alisema watakao patikana watachukuliwa hatua za kisheria.
“Biashara ya madawa inaharibu maisha ya watoto wetu na sisi kama tume ya kupambana na na madawa ya kulevya hatutaruhusu mambo haya kuendelea,” akasema Achenga.
Aidha aliomba serikali za kaunti kuhakikisha kuwa wanaofanya biashara za uuzaji wa pombe hawako karibu na shule.
“Naomba wabunge wetu kukaza sheria inayoonya wauzaji mvinyo kutouza bidhaa hiyo karibu na shule,” akaongeza Achenga.
Kwingineko aliwaomba machifu na manaibu wao kushirikiana ili kupiga vita dhidi ya madawa ya kulevya katika jamii.
Pia aliwaomba kufanya mpango na kusaidia walioadhiriwa na madawa hayo kwa kupewa mafunzo ya jinsi ya kujiepusha nayo.
Kulingana na Achenga wao kama wasimamizi wa tume ya kupambana na madawa ya kulevya wameweka mikakati kabambe na kuomba watu kushirikina na wao.