Fujo iliendelea kushuhudiwa katika bunge la Kaunti ya Mombasa kwa siku ya pili mtawalia baada ya wawakilishi wadi kushikana mashati hadharani.
Mtu mmoja aliripotiwa kuumia vibaya baada ya wingu hilo la fujo kutanda upya huku jaribio la kumng'atua spika wa bunge hilo Thudius Rajwayi likipamba moto.
Haya yanajiri baada ya wawakilishi wadi hao kutofautiana siku ya Jumatano kuhusu uhalali wa fimbo maalum ya spika, iliyokuwa imechongwa kutoka kwa mbao, baada ya fimbo la bunge hilo kuvunjika wakati wa vurugu za siku ya Jumanne.
Mvutano huo ulianza punde spika alipotangaza hatua za kinidhamu zitakazochukuliwa dhidi ya Mwakilishi wa Wadi ya Kongowea Jabez Oduor na mwakilishi wadi mteule Mohamed Khatimy, baada ya kutaka kupigana kufuatia kutofautiana kuhusu swala la kumuondoa Rajwayi.